WELCOME - KARIBUNI SANA

GOD’S PROMISES ARE NEW EVERY MORNING” LAMENTATION 3;23

“All our dreams can come true – if we have the courage to pursue them.” - Walt Disney


Wednesday, April 13, 2016

UKOSEFU WA UADILIFU NA UWAJIBIKAJI


April 13

2 Petro 2:19

Tafakari ya leo tuangalie kwa namna gani ukosekano wa uadilifu na uwajibikaji husababisha watu kutokutekeleza majukumu yao ya kiroho katika namna ambayo inampendeza Mungu;Tatizo kubwa tulilonalo kama Taifa ni ufinyu wa viongozi bora na utashi binafsi wa wachache walio katika nyanja za uongozi kwa kukosa sifa muhimu kwa viongozi. Kwani inatupasa kutambua kuwa uongozi si lelemama, ni kipaji na ni kazi ngumu. Lakini ridhaa hiyo haitolewi hivi hivi tu, inaambatana na amana, kwamba waongozi watatekeleza dhamana  na wajibu  wao kwa makubaliano na maelewano ya kufuata barabara na kuheshimu ipasavyo kanuni na maadili fulani yanayoitambulisha na kuiongoza jamii husika. 

Tafakari yetu inalenga kumwonyesha kiongozi muadilifu jukumu lake ni kufanya kila bidii kuhakikisha amani na utulivu wa kweli katika nchi vinapatikana. Amani na utulivu ni chachu ya wananchi kwa kushirikiana na Serikali yao kujiletea maendeleo. Maendeleo hayaji mahala penye magomvi na hasama. Lakini na amani na utulivu pia haviji mahala pasipo na haki na uadilifu. Uvunjifu wa amani na utulivu wa nchi hupelekea hasara ya maisha na mali ya watu na hayo hayawi malengo ya uongozi muadilifu katika nchi
Maamuzi ya kiongozi wa kisiasa huathiri taifa zima pamoja na ukuaji wa kiroho, busara na hekima huzaa maamuzi yanayotokana na tafakuri ya kina, yanayozingatia hali halisi ya mambo na maslahi na manufaa ya muda mrefu. Kiongozi muadilifu anatakiwa ayaone haya na ayazigatie kwa kila hatua anayochukua. Tukubali tu kuwa njia ya kusonga mbele ni kukubali kutofautiana katika fikra lakini tubaki kuwa wamoja.

Tafakari yetu inasisitiza kuwa kikwazo kukubwa sana cha uadilifu na uwajibikaji ni matumizi mabaya ya ofisi kwa masilahi ambayo hayagusi maisha ya wananchi, rushwa na matumizi mabaya ya pesa ni miongoni mwa malalamiko makubwa katika hoja hii. Rushwa ni miongoni mwa matatizo yanayoikabili dunia nzima kwa ujumla.

Kipimo kimoja kikubwa cha uongozi bora ni uwezo wa kusimamia rasilimali za wananchi, uadilifu, uwajibikaji, uzalendo na kumcha Mungu; kiongozi akiwa na vitu hivi huzaa hekima ua uwajibikaji wa kweli na uzalendo wa kupenda nchi yako na kusimamia rasilimali zake kwa faida ya Taifa.

Tafakari yetu ya leo inatuonyesha kuwa  baadhi ya viongozi wetu kutumia nguvu zao  sio kuondoa umasikini bali kuongeza umasikini kwa mtanzania wa kawaida. Hivyo hata kumletea maisha yake ya Kiroho kuyumba na kuingia katika vitendo ambavyo havimpendezi Mungu. Ni wajibu wa viongozi wetu kuhakikisha kuwa wanatekeleza wajibu wao kwa misingi ya haki na sheria wakikumbuka kuwa hata wao wamechaguliwa na Mungu ili kutimiza adhima ya Mungu Dunia.

Hii ndio tafakari yetu ya leo;

Emmanuel Turuka


No comments:

Post a Comment